YOUTH TECHNOLOGY INITIATIVE

Saturday, September 3, 2011

Liyumba matatani tena, akutwa na simu gerezani




Amatus Liyumba

James Magai
ALIYEKUWA Mkurugenzi wa Utawala na Utumishi (DPA) wa Benki Kuu Tanzania (BoT), Amatus Liyumba ambaye anatumikia kifungo cha miaka miwili jela, ameingia matatani tena akidaiwa kukutwa na simu gerezani aliyoitumia kuwasiliana na Rais Jakaya Kikwete.

Liyumba kwa sasa anatumikia adhabu ya kifungo cha miaka miwili katika Gereza la Ukonga, baada ya kupatikana na hatia ya matumizi mabaya ya madaraka katika ofisi ya umma wakati wa akifanya kazi BoT.

Wakati bado akiwa anaendelea na adhabu hiyo, taarifa zilizopatikana jijini Dar es Salaam jana na kuthibitishwa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ilala, Faustine Shilogile zilisema Liyumba alifikishwa katika Kituo cha Polisi cha Stakishari kilichopo Ukonga na kuhojiwa kwa kosa la kukutwa na simu gerezani.

Habari hizo zilifafanua kwamba Liyumba alifikishwa kituoni hapo saa 3:00 asubuhi kwa gari la Magereza lenye vioo vyeusi na kuhojiwa kwa muda wa takribani dakika 30 kuhusu tuhuma hizo.

Vyanzo hivyo vya habari vilifafanua kwamba, Liyumba anadaiwa kukutwa na simu ambayo ilibaki kituoni hapo kwa ushahidi.

Kwa mujibu wa vyanzo hivyo, Julai mwaka huu Liyumba alimpigia simu Rais Kikwete kwa kutumia simu hiyo. Hata hivyo, bado haijafahamika ni nini hasa alichomweleza Rais lakini habari zaidi zinadai kuwa kitendo hicho kilimfanya mkuu huyo wa nchi kuhoji iweje Liyumba amiliki simu wakati ni mfungwa?
Kutokana na tukio hilo, inadaiwa kuwa maofisa usalama walimwekea mtego na juzi usiku walimdaka akiwa na simu hiyo na asubuhi yake walimpeleka kituoni hapo kwa mahojiano.

“Sasa hivi kinachofanyika ni uchunguzi katika Mamlaka ya Mawasiliano (TCRA) ili kujua alichokuwa akikifanya kwenye hiyo simu na uchunguzi huo ukikamilika basi anaweza kupandishwa kizimbani wakati wowote,” kilidokeza chanzo chetu.

Kifungo cha sasa
Liyumba alihukumiwa kwenda jela miaka miwili na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Mei 24, 2010 na hadi sasa ameshakaa gerezani kwa muda wa miezi 15 na siku 10 (mwaka mmoja, miezi mitatu).

Kabla ya hukumu hiyo, alikuwa amekaa mahabusu kwa muda wa miezi 15 na siku 26 tangu siku aliyopandishwa kizimbani kwa mara ya kwanza, kisha kupelekwa mahabusu kwa kushindwa kutimiza masharti ya dhamana.

Alipandishwa kizimbani kwa mara ya kwanza Januari 27, 2009 akiwa na mshirika wake, Deogratias Kweka wakikabiliwa na mashtaka mawili ya kuisababishia Serikali hasara ya Sh.221bilioni na matumizi mabaya ya ofisi za umma.

Walikuwa wakidaiwa kutenda makosa hayo kwa kuidhinisha upanuzi wa mradi wa majengo pacha ya BoT, bila idhini ya Bodi ya Wakurugenzi na hivyo kuongeza gharama za mradi tofauti na zilizoidhinishwa na bodi.

Hata hivyo, baadaye Kweka alifutiwa mashtaka na kubakia Liyumba peke yake ambaye naye alishinda kosa kubwa la kuisababishia Serikali hasara ya Sh.221bilioni na kubaki na kosa la matumizi mabaya ya madaraka ambalo lilimtia hatiani.

Mei 28 mwaka huohuo, kwa kutumia jopo la mawakili walioongozwa na Majura Magafu, Liyumba alikata rufaa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es salaam akitoa sababu 12 za kupinga hukumu hiyo pamoja na adhabu.
Katika sababu zake za kupinga hukumu hiyo jopo la mawakili wa Liyumba pamoja na mambo mengine, lilisema Mahakama ya Kisutu ilikosea kisheria na kiukweli katika kutathmini ushahidi na utetezi.

Hata hivyo, Desemba 21, 2010, Mahakama Kuu ilitupilia mbali rufaa yake na kukubaliana na hukumu iliyotolewa Mahakama ya Kisutu.

Friday, August 26, 2011

Dereva anayedaiwa kuua mbunge, mkewe ashtakiwa
HOSPITALI ya Taifa ya Muhimbili (MNH) Kitengo cha Mifupa (MOI), jumatano(tarehe 24) iligeuka kuwa mahakama kwa muda baada ya dereva wa aliyekuwa mbunge wa Jimbo la Uzini, Chezard Sebunga (31), kusomewa mashtaka matatu akiwa chini ya ulinzi hospitalini hapo.

Sebunga, ambaye ni mkazi wa Dodoma na dereva wa aliyekuwa Mbunge wa Baraza la Wawakilishi (CCM), Mussa Silima, alisomewa mashtaka matatu likiwamo la kusababisha vifo vya watu wawili; mbunge na mkewe na kujeruhi abiria kutokana kuendesha gari kwa uzembe.

Sembunga anadaiwa kusababisha ajali hivi karibuni, eneo la Nanenane-Nzuguni barabara ya Dodoma Morogoro na kusababisha watu wawili kupoteza maisha na mwingine kujeruhiwa.
Mshtakiwa huyo amelazwa wodi maalumu chumba namba mbili, baada ya kuvunjika mguu wa kulia mara tatu na kuwekewa chuma.

Katika ajali hiyo, mshtakiwa anadaiwa akiendesha gari aina ya Toyota Coralla aligongana na lori, kisha kuhama njia na kugonga Scania lililokuwa upande wa pili wa barabara.

Alidaiwa kusababisha vifo na kuendesha gari kwa mwendokasi na kusababisha abiria Salma Juma kujeruhiwa.
Mwendesha Mashtaka wa Serikali, Nassoro Katuga, alidai mshtakiwa alitenda makosa hayo Agosti 21, mwaka huu barabara ya Dodoma -Morogoro eneo la Nanenane Nzunguni, Manispaa ya Dodoma.

Mwanga alidai siku ya tukio saa 9:00 alasiri eneo hilo, akiwa na gari hiyo aina ya Toyota Corolla anadaiwa kuendesha gari kwa uzembe baada ya kushindwa kutumia tahadhari na kusababisha kifo cha Mwanaheri Mwaibu.
Aliendelea kuwa mshtakiwa akiwa dereva aliendesha gari kwa mwendokasi na uzembe bila tahadhari na kusababisha kifo cha Mbunge wa Baraza la Wawakilishi Jimbo la Uzini, Mussa Silima.

Katika shtaka la tatu, mtuhumiwa siku na wakati huohuo anadaiwa kumjeruhi abiria, Salma Juma.
Mshtakiwa alikana mashtaka na Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Ilala, Joyce Minde, aliahirisha kesi hiyo hadi Septemba 8, mwaka huu itakapotajwa tena.Minde alisema mshtakiwa atafunguliwa mashtaka upya atakapopelekwa Dodoma.
Makinda ambana Waziri Muhimbili kukatiwa umeme
SPIKA wa Bunge Anne Makinda jana alimbana Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Adam Malima akimtaka atoe maelezo ni kwa nini juzi umeme ulikatika katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH).Makinda alimtaka Naibu Waziri kutoa sababu za msingi za kukosekana kwa huduma ya umeme katika hospitali hiyo akisema ni jambo la hatari kwa afya za wagonjwa.

Juzi, iliripotiwa kuwa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili haikuwa na huduma za umeme na maji jambo lililosababisha kero kwa wagonjwa na kukwamisha baadhi ya huduma muhimu.“Mheshimiwa Naibu Waziri, hebu eleza hata Muhimbili hakuna umeme wala maji, hilo nalo unawaambiaje Watanzania?’’ alisema Makinda.Swali hilo lilimpa wakati mgumu Malima kulijibu akisema hata yeye hajui sababu za taasisi hiyo nyeti kukatiwa umeme.

Malima alitaja sababu za Jiji la Dar es Salaam kukosa umeme kuwa ni pamoja na matatizo katika Gridi ya Taifa ambapo Megawati 150 zilikosekana katika siku za karibuni lakini akasema hicho siyo kigezo cha kuifanya Muhimbili ikatiwe umeme.

“Mheshimiwa Spika, nataka niseme hapa kuwa kwenye Gridi ya Taifa kulikuwa na tatizo lililolifanya Jiji likose umeme wa megawati 150 hivi, lakini hata hivyo, hiyo siyo sababu ya kufanya Muhimbili wakose umeme labda kuna tatizo jingine naomba unipe muda nifuatilie nitatoa jibu la uhakika,’’ alisema Malima.

Naibu Waziri alisema tatizo kubwa katika hospitali hiyo halikutokana na uzalishaji, bali alihisi kuwa vipo vyanzo vingine ambavyo hata hivyo hakuweza kuvibainisha.


Hali ya Muhimbili
Leon Bahati na Godfrey Nyang’oro, wanaripoti kuwa huduma kwa wagonjwa wanaotibiwa na kulazwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili imezorota kutokana na kukatika na umeme mara kwa mara kwa siku ya tatu mfululizo.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti wauguzi, wagonjwa na waganga wa wadi za Mwaisela na Sewa Haji, katika hospitali hiyo walisema kwamba, hali ni mbaya zaidi katika wadi za wagonjwa ambazo hazipati umeme wa jenereta.

Mmoja wa wauguzi ambaye hakutaka kutaja jina lake kwa kuhofia ajira yake alisema kuwa, wodi ya Sewa Haji ipo giza badala yake wanatumia taa za chemli na kwamba, kutokana na hali hiyo wanapata wakati mgumu kukabiliana na msongamano wa wagonjwa.

Muuguzi huyo alisema tangu ulipoanza kukatika umeme siku mbili zilizopita, maeneo yote ya wodi hayana umeme. “Mapokezi na maabara wanatumia umeme wa jenereta na wodini hakuna, tunatumia taa za kawaida,” alifahamisha muuguzi huyo.

Mwananchi lilipotembelea Muhimbili lilishuhudia mafundi wa Shirika la Umeme nchini (Tanesco) wakiendelea na ukarabati wa nyaya katika baadhi ya maeneo.

Ofisa Uhusiano wa Taasisi ya Mifupa (Moi), Almasi Jumaa, alisema kwamba kwa upande wa taasisi hiyo hali ni shwari kwa sababu wana jenereta za kutosha ambazo huzitumia umeme wa Tanesco ukikatika.

"Hatuna tatizo kwa upande wa Moi. Sisi kama taasisi inayojitegemea tuna jenereta ambazo wakati wote ziko tayari kufanya kazi mara umeme unapokatika," alisema Almasi.

Ofisa Habari wa MNH, Aliamini Aligaesha, alikiri hospitali hiyo ilikosa umeme kwa siku tatu mfululizo kutokana na matatizo ya kiufundi kwenye mtandao wa usambazaji ndani ya hospitali hiyo.

Alisema kwamba, siyo kawaida kwa hospitali hiyo kupata mgawo wa umeme tangu matatizo ya nishati hiyo yalipoanza nchini, lakini kwa siku tatu hali ilikuwa mbaya.

Alisema waliweza kukabiliana na tatizo hilo kwa kuwasha jenereta isipokuwa wodi tatu za Sewahaji, Mwaisela na Kibasila, ambazo hazina jenereta hivyo zilibakia gizani na kwamba badala yake watumia taa za chemli na zinazotumia umeme wa kuchaji.

Aligaesha alifahamisha kuwa umeme ulikatika Jumatano iliyopita na mafundi wa Tanesco na MNH wanashirikiana kutatua tatizo hilo.

" Hapa umeme ulikatika Jumatano saa 1:00 jioni. Tuliwaita Tanesco, walipofika waligundua hitilafu ya umeme kwenye njia kubwa wakairekebisha. Ilipokamilika tukaunganisha, lakini baadaye tukagundua kuna tatizo upande hospitali," alisema Aligaesha.

Aliwatetea mafundi wa Tanesco kwamba huwa wanatoa ushirikiano wa hali ya juu kutatua tatizo la umeme kila linapotokea hospitalini hapo, lakini hilo limeonekana kuwa zito na linahitaji umakini zaidi.

Alisema menejimenti ya MNH inajitahidi kukabiliana na tatizo hilo kwa kununu jenereta maalumu kwa ajili ya majengo hayo matatu.

"Unajua Muhimbili tuna majengo karibu 20 na yote yanahitaji kuwa na jenereta. Hata hizo wodi tatu tunaamini baada ya muda yatawekea jenereta," alisema Aligaesha.


Gaddafi atoa ujumbe akiwa mafichoni, vikosi vyake vyajibu mapigo
TRIPOLI, Libya
VIKOSI vya jeshi vinavyomtii Kiongozi wa Libya, Muammar Gaddafi, jana vilikutana uso kwa uso na kupambana vikali na vikosi vya waasi na vile vya Umoja wa Kujihami Nchi Magharibi (Nato).

Gaddafi, ambaye anatafutwa na waasi kwa nguvu zote, juzi walitangaza zawadi ya dola 1.7 milioni za Marekani (Sh2 bilioni) kwa mtu yeyote atakayewezesha kukamatwa, au kumuua Gaddafi.Habari zinasema Gaddafi alitoa ujumbe akiwa mafichoni akivitaka vikosi vyake vyote vya jeshi, ambavyo vilipunguza kasi ya kupigana vijibu mashambulizi waliopo mjini Tripoli.

Vikosi hivyo vinavyomtii Gaddafi katika hatua ya kuurudisha uwanja wa ndege wa kimataifa unaoshikiliwa na waasi, jana vilipigana vikali na waasi kwenye uwanja huo ambao ndiyo mkubwa nchini humo.

Hata hivyo, waasi hao bado wanajigamba kuwa mji wa Tripoli tayari wameudhibiti. Usiku wa kuamkia jana milio ya risasi na milipuko ya mabomu ilitikisa mji wa Tripoli hasa uwanja huo wa ndege, ambao mpaka hivi sasa unashikiliwa na waasi.

Nato walenga handaki la Gaddafi
Wakati Gaddafi anatoa ujumbe wa kuendeleza mapambano, ndege za Nato jana zilishambulia kwa kurusha mabomu kwenye handaki kubwa lilikopo mji wa Sirte, alikozaliwa kiongozi huyo.

Ndege hizo ziliondoka kambi ya jeshi iliyopo Nolfolk siku ya Alhamisi usiku.Hata hivyo, waasi wa Libya nao wanaimarisha majeshi yao kwenye barabara inayoelekea Sirte, wakipeleka vifaru na makombora.

Wakati huohuo, Umoja wa Ulaya (EU) umesema utapeleka misaada ya haraka ya dawa kwenye hospitali zilizofurika wagonjwa, ambako hali inaarifiwa kuwa mbaya.

Waasi wahamia Tripoli
Baraza la Mpito la Kitaifa la limeondoka Benghazi na kuhamia Tripoli. Naibu Mwenyekiti wa Kamati ya Utendaji, Ali Tahuni, alisema baraza hilo limeanza kufanya kazi mjini humo.Baraza la Mpito la Kitaifa, limeahidi kuwasamehe wanajeshi na wanamgambo waliokuwa wakimpigania Gadaffi, ikiwa wataweka silaha chini.

Gaddafi bado yupo mafichoni
Bado haijulikani mahali alipo Kanali Gaddafi na familia yake. Katika hatua nyingine, Rais wa Afrika Kusini, Jacob Zuma, amezishutumu nchi za Magharibi kwa kukiuka azimio la Umoja wa Mataifa dhidi ya Libya.Kwa upande mwingine bila ya kujali iwapo Kanali Gaddafi atakamatwa au la, mkutano wa kimataifa kwa ajili ya kujenga upya Libya umepangwa kufanyika Septemba Mosi.

Naye Msemaji wa waasi, Abdel Salam Abu Zaakouk, alisema mazungumzo yanaendelea kati yao na viongozi wa makabila maeneo mbalimbali kutafuta suluhu ya mzozo huo.

Alisema uongozi wa waasi uliahidi kukubali Kanali Gaddafi aondoke salama nchini humo kwa kuachia madaraka.
Lakini, kiongozi huyo wa Libya ambaye hajulikani aliko aliapa kupitia hotuba iliyorushwa kupitia redio moja ya kitaifa kwamba, yuko tayari kupigana hadi ashinde au afe.

UN yaidhinisha fedha
Umoja wa Mataifa (UN) umetoa idhini ya kuziachia dola 1.5 bilioni za Gaddafi zilizozuiliwa. Fedha hizo zitatumiwa kwa misaada ya kiutu kwa nchi hiyo iliyokumbwa na mapigano.

Kwa mujibu wa uamuzi wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, fedha hizo zinatazamiwa kusaidia Serikali kujenga upya Libya kufuatia mapigano ya miezi kadhaa.


Wednesday, August 24, 2011

GADDAFI: NITAPAMBANA HADI KIFO.......!

Waasi wakikanyanga picha ya Gaddafi
Kanali Muammar Gaddafi ameapa kupigana na waasi hadi kifo au ushindi, ripoti zimesema, baada ya waasi kudhibiti makazi yake mjini Tripoli.
Televisheni inayomuunga mkono Kanali Gaddafi, al-Urubah, imesema Kanali Gaddafi ambaye bado hajulikani alipo, ametoa hotuba akisema kuondoka kutoka kwa makazi yake kulikuwa ni ''mpango''.
Makazi hayo ndiyo yaliyokuwa maeneo ya mwisho chini ya udhibiti wa Kanali Gaddafi mjini Tripoli.

Waasi wamekuwa wakisheherekea mafanikio yao katika bustani ya Green Square, mjini Tripoli.
Sanamu ya Gaddafi yaharibiwa. 
Picha za televisheni pia zimeonyesha wapiganaji wakivunja sanamu ya kiongozi huyo na kuipiga mateka baada ya kuuteka Bab al-Aziziya siku ya Jumanne. Waasi hao pia walichukua vifaa mbalimbali katika makazi hayo ya Kanali Gaddafi.
Hata hivyo bado mapambano yanaripotiwa katika mji huo, mkiwemo katika maeneo ya Abu Salim na Hadba na karibu na hoteli ya Rixos, ambapo waandishi wa kigeni wanapoishi.
Mwandishi wa BBC Rana Jawad mjini Tripoli amesema kuwa kuna hisia kuwa huu ndio mwisho wa utawala wa Kanali Gaddafi, lakini sherehe kamili hajitaanza hadi pale yeye na jamaa wake watakapo kamatwa.
Akizungumza na redio moja mjini Tripoli, Kanali Gaddafi ameahidi''kifo au ushindi'' katika mapigano dhidi ya majeshi ya NATO na waasi wa Libya, redio ya al-Urubah ilisema.

Kanali Gaddafi aidha amesema makazi yake yameharibiwa na mashambulio 64 ya angani ya NATO.
Jumanne asubuhi, wapiganaji wa waasi waliokuwa wamejihami vilivyo walimiminika katika mji mkuu kushiriki katika mashambulio ya Bab al-Aziziya.
Baada ya saa tano ya mapigano makali, walivunja lango kuu na kuvamia makazi hayo.
Waasi walionekana wakiharibu masanamu, mkiwemo sanamu ya dhahabu, ya mkono unaovunja ndege ya kivita ya Marekani. Hema ya Kanali Gaddafi ambayo aliitumia kupokea wageni pia iliteketezwa.
Wametoroka kama panya.

''Tumeshinda makabiliano'' Abdul Hakim Belhaj, kamanda wa ngazi ya juu wa waasi mjini Tripoli aliliambia shirika la al-Jazeera.''Wametoroka kama panya''.
Haijulikani iwapo kanali Gaddafi na jamaa wake walikuwa katika makazi hayo ya Bab al-Aziziya, lakini inaripotiwa kuwa ina mahandaki ya chini kwa chini, yanayounganisha na maeneo mengine ya mji.
Hali sio wazi katika mji wa Sirte, alikozaliwa Kanali Gaddafi, ambayo imekuwa ngome ya maafisa wanaomuunga mkono. Ripoti zinasema wanajeshi waliorudishwa nyuma wanaelekea huko.